Saturday, December 10, 2016

Kamata sana hii elimu

Katika elimu ambazo zinaogopwa ni hizi zinzohusu masuala ya ulemavu. Mtu anahisi akiifuatilia anaweza akaupata ulemavu. Hakika ulemavu unawapata watu, lakini si wote wanaweza kuathiriwa na ulemavu kwa kiwango kinachofanana. Ugumu unakuja kuwa "ni nani anayefuata kwa kupata ulemavu (kwa wasio na ulemavu)?"

Umuhimu wa elimu hii upo hapa:
1. Hii ni elimu ihusuyo afya ya mwili wako
2. Elimu hii inasaidia kuepuka mazingira hatarishi ya kupata ulemavu wa aina fulani fulani (mfano: ulemavu unaotokea kwa kutozingatia lishe bora).
3. Elimu hii juu ya ulemavu inasaidia kuwa na mtazamo chanya juu ya binadamu wengine wenye ulemavu.
4. Elimu hii ni sawa na huduma ya kuganga mioyo ya watu walioathiriwa na ulemavu kwa namna moja ama nyingine. Nimejifunza mambo mengi juu ya jamii ya watu wenye ulemavu na familia zao.

Ushuhuda wa kweli:
Kuna siku nikiwa natembea mtaani nilisimama kusalimiana na jamaa zangu. Mtu mmoja akasema "mtu yule mbona anaachwa kutambaa mtaani kwa shida"?. Huyu jamaa yangu alimaanisha kuwa ni kitendo cha aibu sana kwa mtu mwenye ulemavu kuonekana mtaani. Mimi nilianza kwa kusema: Hawa watu wanaokaa na huyu mtu wana akili sana, wana utu na wanampenda mtu wao. Nikamalizia kwa kusema: "Ulemavu ukiupokea vibaya unaweza ukawa masikini".
Katika kundi lile alikuwepo jamaa ambaye alishaathiriwa na ulemavu wa mwanae kwa miaka kadhaa. Akanishika mkono akanipeleka pembeni na kuanza kunihoji.

Miongoni mwa mambo aliyoniambia ni kuwa amehangaika na huyo mwanae kwa waganga hadi akafilisika, amekimbia kutoka Arusha na kwenda Morogoro kwa kuogopa aibu kwa marafiki zake. Akaongeza kusema kuwa mwanae huwa anamfungia ndani akienda kufanya shughuli zake. Nilipomwelekeza namna ya kuishi na huyo mwanae mwenye ulemavu alinielewa na kuishia kusema "mzigo nimeutua sasa".

Wapo watu wengi waliokosa huduma kama hizi, wanapata shida kwa kutokujua jinsi ya kuishi na jamii za watu wenye ulemavu na pia kupata shida ya kujifikiri juu ya ulemavu wao.
5. Ni elimu inayomhusu mtu mwenye ulemavu ajikubali jinsi alivyo, watu wanaotunza wenzao wenye ulemavu wasijisikie vibaya na kuwajengea utamaduni watu wasio na ulemavu jinsi ya kufikiri kivingine bila kuzingatia mapokeo mabaya juu ya watu wenye ulemavu. Ni kweli kila apataye ulemavu amelaaniwa? Amefanya kosa? Kwanini atengwe? Kwanini aonekane si binadamu? Ndiyo aonekane hawezi? (Haya ndiyo ya kujirekebisha).

Naendelea kukutia moyo wa kusoma maandiko haya kila upatapo nafasi ya kufanya hivyo.


Tengeneza Maana kwenye uwanja wa fujo






Utamaduni una nguvu kwenye maisha ya binadamu, naam, ndiyo maisha yenyewe! Tunaishi kutokana na utamaduni tuliojiwekea.

Jamii nyingi za Kitanzania hazipendi kufanya mijadala juu ya watu wenye ulemavu. Huu ni utamaduni wa jamii zetu katika ngazi za kaya, ukoo, kabila na hata kuakisi taifa zima.

Kutokana na utamaduni huu wa kutokufanya mijadala mingi juu ya ulemavu na watu wenye ulemavu kuwa ni mwiko (taboo) kuongelea masuala ya ulemavu. Kutoka hapa ndipo pamezaliwa, kukua na kukomaa kwa mizizi ya unyanyapaa kwa watu wenye mahitaji maalum.

Kama taifa, tunahitaji watu wenye roho ngumu za kutengeneza maana ya maisha kwa watu wenye mahitaji maalum na kwa watu wote ambao kwa namna hii au ile wameathiriwa na ulemavu (mfano: wazazi na walezi wenye watoto wenye ulemavu). Tunahitaji watu watakaotoa huduma ya kuwawezesha wahanga hawa kupumzika kisaikolojia (psychological comfort). Huduma hii ni adimu sana hapa nchini.

Kama kwenye vita za risasi na mabomu wapo watu wenye kujipatia ajira kwa vita hizo (mfano waandishi wa habari), je, si rahisi sana kupata ajira ya kutangaza habari za amani, mshikamano na upendo ndani ya nchi yetu wenyewe? Naam, inawezekana!

Wapo watu wengi wenye mahitaji maalum ambao wanatafuta neno la kuambiwa 'unaweza' na hawapati. Wapo wazazi na walezi ambao wanataabika kisaikolojia kwa kutokujua namna ya kukaa na watoto wao wenye mahitaji maalum- wanashindwa kupata mtu wa kusema 'mwanao ni mzuri na anaweza kufanya abcs'.

Sote tufikiri juu ya hilo!



Thursday, April 14, 2016

The Vantage Points towards disability

Unaware Moments!
Sometimes we do not consider others in a community programs not just we don't like them! The situation occurs due to the inbuilt consciousness in our minds. This is, exactly what keeps disturbing our fellows with disabilities around the world. Perception over people with disabilities and disability issues do not depend on how man is educated or his richness, illiterate and professors fall the same category! Of course, these people share the same vantage angles through which disabled people are determined. They both put aside their learned environmental knowledge and ware artificial thoughts. Indeed,  both are led by uncontrolled emotions! They fail to analyze the causes and effects of disability to an individual, they fail to set the line of demarcation between faith and facts! People with disabilities are, in most cases placed in spiritual affairs. They are always thought of being cursed, punished, have something to do with ancestors!

However, it should be noted that all human beings have 9+ talents created innately. They hastily forget that the nation can be built by both people with and without disabilities.

See Ability beyond disability
Figure out what a person is able to...
Think about them in a human face...
Just use facts to think inclusively!

Sunday, April 10, 2016

JE, WAJUA ATHARI ZA ULEMAVU KWA MAISHA YA MTU?




Kwa asilimia kubwa, ulemavu wenyewe sio tatizo, bali mtazamo wa jamii juu ya ulemavu huo ndio tatizo kubwa zaidi. Ukiacha ulemavu unaohusisha ubongo, ulemavu mwingine wote una faida ya kumwongezea akili nyingi mhusika mwenye ulemavu. Anakuwa na maisha ya utafiti wa kila siku juu ya tabia za binadamu na utamaduni wao. Ulemavu unaleta hamasa ya ugunduzi wa asili wa binadamu na tabia zake.
Hata hivyo, maisha ya ulemavu yamejaa kuanguka na kusimama kwa nyakati tofauti kutokana na tamaduni kinzani juu ya ulemavu na watu wenye ulemavu. Nafsi rahisi (easy minds) za watu wenye ulemavu na washirika wao huanguka kwa anguko kubwa kwenye maisha ya kila siku. Hii inatokana na uzito na ugumu wa taratibu za mila na desturi kwenye jamii zetu. Pia kumbuka kuwa ukiona mtu shujaa mwenye ulemavu kwenye kila jambo ujue kapigana kwa nguvu zana ili kushinda mapito hayo. Mtu mwenye ulemavu hukutana na maneno makali yenye kukatisha tama, vitendo vya ukinzani, mitazamo kinzani kama tufani ya bahari, kila hatua ya makuzi na maisha yake ni ukinzani tupu. Ndio maana kuna makabila fulani ya kitanzania wakiona dalili ya ulemavu kwa mtoto mchanga wanamuua siku ile ile ya kwanza kwa kisingizio kuwa si “riziki”.
1. Athari ya kiuchumi
Familia nyingi zenye watoto wenye ulemavu, hasa wa akili zinakumbwa na ugumu kiuchumi kwa kuwa muda mwingi wanatakiwa wawe na watoto wao wenye ulemavu. Hali hii inapelekea wazazi hao kuacha kazi zao za kiuchumi. Zipo shuhuda nyingi kwa watu ambao nimepata kuongea nao wenye watoto wenye ulemavu.
2. Athari za kijamii
Jamii zetu zina mtazamo hasi juu ya ulemavu. Mtu mwenye ulemavu amekosa sifa kwenye jamii, anaonekana ni mtu tegemezi, hana haki, mnyonge, amelaaniwa na matokeo yake ni kutengwa na jamii yake. Nimeona watu wengi ambao kabla ya kuwa na ulemavu walikuwa maarufu kisiasa, kiuchumi na kijamii, lakini mara walipopata ulemavu “status” zao zilibadilika.
3. Athari za kimazingira
Watu wenye ulemavu wa aina mbalimbali wanatakiwa watengenezewe njia wezeshi kwa maisha yao, yaani “deviated programs and means for people with disabilities”. Tumepungukiwa vifaa jumuishi. Mazingira mengi ya watu wenye ulemavu ni changamoto.
4. Sera za nchi
Zipo sera za watu wenye ulemavu na zingine kama miongozo kwa maisha ya wananchi kwa ujumla. Sera za watu wenye ulemavu ni ngumu kutekelezeka, na zile jumla hazina dalili ya ukaribu na mtu mwenye ulemavu.
Ushuhuda: Kuna rafiki mmoja ambaye ni mwalimu kipofu. Aliomba kazi ya kufundisha kwenye shule ya binafsi, kwa vile ufaulu wake ulikuwa mzuri walimwita kwenye usaili. Alipofika wakamwona kipofu, wakamwambia kwa kimombo”we need a teacher but not you, sorry for that.” Wakaongeza kusema: “Hatukujua kama wewe ni kipofu”.
Kiukweli ipo mifano mingi ya aina hiyo!
5. Utu wa mtu mwenye ulemavu
Fanya jaribio la uchunguzi: Fuatilia mahali ambapo ghafla ametokea mtu mwenye ulemavu usikie maneno ya watu juu yake. Hata kama hawasemi chochote utaona “facial expressions” zao tu. Kiukweli utagundua ya kuwa kwa mitazamo ya jamii zetu mtu mwenye ulemavu anawekwa kwenye jamii ya upili. Kila mtu hufikiri ana mamlaka juu ya mtu mwenye ulemavu, mtu mwenye ulemavu hakui kwenye jamii, siku zote hufikiriwa ni tegemezi, ana akili za kitoto, na kila afanyacho huonekana si sahihi.
Ugumu kwa wapatao ulemavu ukubwani ni ile hali ya kuzoea aina mpya ya maisha. Marafiki hupungua, imani ya watu kwake hupungua. Hii hali huwafanya watu hawa wenye ulemavu kuishi maisha ya simanzi siku zote.
Ushuhuda
Mwanafunzi wangu mmoja wa zamani alipata ajali na kukatwa mguu (unyayo wote), amekuwa na mazingira magumu sana. Amekuwa ni mtu wa kutoa machozi tu akifikiria ugumu anaoupata.


Usione shida kwa msisitizo ambao huwa nautoa kila siku juu ya mambo ya watu wenye ulemavu. Ukichunguza kwa makini haya madhara ya mtu kuwa na ulemavu unakuta mtu asiye na ulemavu anaogopa neno “ulemavu” kuliko ulemavu wenyewe. Akisikia habari za ulemavu na watu wenye ulemavu anahisi masikio yanapata kuumia. Kwa hakika, ulemavu unamgusa kila mtu kwa namna yake.
Je, ulishawahi kujiuliza mapito ya watu albino nchini? Mapito ya watu albino na watu wenye ulemavu mbalimbali ndiyo sababu kubwa inayonifanya niendelee kuzungumzia masuala ya ulemavu kwa kadri Mungu anavyoniwezesha kuwa na uhai kwa manufaa yetu sote. Tujifunze juu ya ulemavu, tujifunze tunavyoweza kuishi na ulemavu na/au watu wenye ulemavu.

Tufikiri Kijumuishi…..Tutende Kijumuishi……Tujenge Taifa Jumuishi…

Muondolee mwanao athari za ulemavu

Maamuzi unayofanya leo juu ya mwanao ndiyo hatima ya maisha yake ya baadae. Maisha yake ya baadae yatakuwa ni matokeo ya maamuzi utakayomfanyia leo juu ya maisha yake. Maisha yetu ni matokeo ya maamuzi yaliyofanywa juu yetu na watu wengine.

Kabla ya kuzaliwa

Mama mjamzito afuate na kuzingatia maelekezo yote ya kitabibu juu ya ujauzito wake. Kula vyakula stahiki na fanya mazoezi sahihi kwa makuzi bora ya mtoto tumboni. Upo uwezekano wa mtoto kuzaliwa akiwa na ubovu wa mifupa, kuharibika akili, kulemaa viungo nk.
Club foot (Kifundo mguu)

Wakati wa kuzaliwa
Fuata maelekezo ya madaktari ili mtoto wako azaliwe kwa wakati husika. Usisahau kumwomba Mungu ili awe nawe wakati huu. Mtoto akichelewa kuzaliwa kwa wakati na kwa kutumia vifaa saidizi kuna madhara ya kuharibiwa ubongo wake.

Wakati amezaliwa
Hakikisha unamlinda mwanao na vihatarishi vyote juu ya ulemavu unaoweza kumpata mwanao. Mfano: Epuka kumpa mwanao vifaa vyenye ncha kali kama sindano ambavyo vinaweza kutoboa macho na masikio, Epuka uwezekano wa kumwangusha mwanao (anaweza kulemaa akili na viungo), epuka kukaa na mwanao maeneo yenye kelele (ili kuepusha ukiziwi na kukosa utulivu-Hyperactivity). Epuka kumweka mtoto kwenye mchanga kama ule wa kupigia sakafu za nyumba. Ni hatari kwa macho ya mtoto. Upo ushuhuda mwingi juu ya watu waliopata upofu kupitia mchanga.
Pia mchunguze mwanao viungo vyake baada ya kuzaliwa. Kuna ulemavu uitwao "Club foot" au "Kifundo mguu" ambapo mtoto anakuwa na unyayo uliojikunja, matege yasiyo kawaida. Ukigundua mapema mpeleke mwanao hospitali kwa tiba zaidi.

Haya niliyoyataja na yale ambayo sikuyataja na mengine mengi unayoyafahamu yazingatie sana kwa ustawi wa maisha ya mwanao.

Msisitizo: Ulemavu una athari kubwa kwa mtu mwenyewe mwenye ulemavu, familia yake na hata ukoo wake. Athari hizi zinahusisha nyanja za kiuchumi, kisiasa, kijamii na kiutamaduni kwa ujumla wake.

Najiandaa kukuletea mada ya athari za ulemavu kwenye maisha!

Fikiri Kijumuishi.....Tenda Kijumuishi..... Jenga Taifa Jumuishi......

Unauelewaje Ulemavu?



Kwanza kabla ya yote niseme tu kuwa ukiona mtu anaelewa haraka juu ya mambo ya watu wenye ulemavu ujue kuwa kwa namna moja au nyingine aliwahi kupata aidha kwa ndugu wa karibu mwenye ulemavu na/au ana rafiki mwenye ulemavu.
Watu wengi ambao nimeongea nao inonyesha kuwa walishaguswa na huu ulemavu, iwe kwa watoto wake, wazazi wake, wenzi wao, na watu wao wengine ambao ni wa karibu sana. 

Nimegundua kuwa masuala ya ulemavu hayazungumzwi sana kwenye jamii kutokana na tamaduni zetu.
Watu wamefanya ulemavu kuwa ni siri kubwa. Watu wengi wenye ndugu zao wenye ulemavu wanawafungia ndani ndugu hao wenye ulemavu, wamewakosesha fursa ya elimu na haki ya kuchangamana na jamii. Hii ni kwa sababu elimu juu ya watu wenye ulemavu na ulemavu wenyewe haitiliwi mkazo. 

Watu wengi wakishindwa kutafsiri masuala ya ulemavu kitaalam hujikita katika imani za dini, na kishirikina. Wengi kwa imani huamini kuwa mtu kupata ulemavu ni laana ya ukoo. Wababa wengi wamewakimbia familia zao (wake wao wazaao watoto wenye ulemavu) zenye watoto wenye ulemavu.

Kwa hakika ulemavu umetafsiriwa na binadamu kwa ajili ya binadamu. Kila binadamu ni mhanga wa ulemavu. Tuvumiliane, tuheshimiane, tusaidiane inapobidi, tuuangalie uthamani wa binadamu na ubinadamu wake. Ulemavu ni sehemu tu ya haiba ya mwanadamu.

Je, una mtoto mlemavu?, rafiki mlemavu?, mzazi mlemavu?, mwenzi mlemavu? au wewe mwenyewe una ulemavu?

Usijali maneno na mitazamo ya watu wengine juu ya ulemavu huo. Ishi kwa kadri ulivyojizoeza!

Fikiri Kijumuishi...Tenda Kijumuishi....Jenga Taifa jumuishi!

Sunday, March 13, 2016

Tupunguze viashiria vya ulemavu

Katika dunia ya leo, asilimia kumi ya kila idadi ya watu kadhaa ni watu wenye ulemavu.
Ulemavu upo wa makundi mawili,; wa kuzaliwa nao (congenital) na ule aupatao mtu akiwa amezaliwa (acquired). Pia ulemavu unaweza kuwa wa kurithi kutokana na vinasaba vya mtiririko wa kizazi husika.

(A) Namna ya Kupunguza ulemavu

Ulemavu wa kuzaliwa (ambao si wa kurithi)
1. Mama mjamzito fuata kanuni za kitabibu kwa kupata virutubisho sahihi kwa makuzi ya ujauzito wako
2. Baba epuka kuleta ghasia kwa mama mjamzito kama vile kumpiga mateke ya tumbo, kuwa mkali kwa mke wakati wa ujauzito wake.
3. Baba na mama mshirikiane ili kuhakikisha mimba inakua vizuri hadi hapo mtoto atakapozaliwa
4. Daktari awe wazi kuwataarifu wazazi watarjiwa wa mtoto pale anapobaini kuna dalili za ulemavu kwa mtoto ili kuona kama uwezekano wa kupunguza athari za ulemavu huo. Mfano, mtoto anayezaliwa na kifundo cha mguu (Club foot) anaweza kurekebishwa miguu yake angali mtoto mchanga.
5. Baba na mama muishi maisha ya furaha, hasa baba jitahidi kumjengea mama mjamzito furaha kubwa.

(B) Ulemavu baada ya kuzaliwa
Ulemavu wa aina hii ni matokeo ya ajali mbalimbali kwenye mazingira yetu
1. Epuka kugongeshagongesha kichwa cha mtoto mchanga ili kuepuka kuharibu ubongo wa mtoto (mtindio wa ubongo)
2. Epuka kukimbilia kwa waganga wa kienyeji kwa tiba isiyo ya lazima kwa watoto. Kituo cha kwanza kwa matibabu yoyote ya mtoto iwe kwa madaktari waliosomea udaktari. Huko kwingine iwe ni ziada tu (hii itasaidia kitaalam kujua maendeleo ya afya ya mwanao.
3. Epuka kumpa mtoto wako vifaa vyenye ncha kali kama vile sindano, mouth sticks, kalamu za wino, visu nk. Vifaa hivi ni hatari kwa macho na masikio ya mtoto (upofu na ukiziwi au vyote kwa pamoja).
4. Epuka kumweka mwanao kwenye mchanga. Mara nyingi ni hatari kwa macho ya mtoto.
5. Epuka kumtishia mtoto mdogo kama vile tusemavyo kwa vitisho. Hii huweza kumsababishia mtoto kuwa na vurugu za maono, hasa hasira na woga uliopitiliza kiasi cha asili ya binadamu.
6. Epuka kumpiga makofi mwanao; unaweza ukamharibu masikio na mishipa ya macho na kumsababishia upofu na ukiziwi.
7. Epuka kuishi maeneo yenye kelele nyingi kama vile viwandani, migodini, vituo vya mazoezi ya kulenga shabaha kwa wanajeshi, karibu na viwanja vya ndege. Hii husababisha ukiziwi kwa mtoto.

(C) Ulemavu wa kurithi
Hapa sasa niongee na vijana ambao hawako kwenye ndoa.
Mara nyingi ulemavu wa kurithi ni matokeo ya kuwepo kwa vinasaba vya ulemavu husika kwa wana ndoa.
Ili kuepuka na/au kupunguza huu ulemavu ni jukumu lako kijana ambaye hujaoa au kuolewa kufanya uchunguzi wa kina juu ya mwezi wako mtarajiwa.
1. Uliza kama kwenye ukoo wao kuna ulemavu wa kurithi, na kama upo, je, unaweza ukaathiri kizazi chenu? Upo ulemavu wa kurithi ambao akiwa nao mmoja wa wana ndoa hauwezi kuathiri kizazi chenu.
2. Anza maandalizi ya uchunguzi wa huyo unayependa awe mwezi wako kabla ya kumdokezea kuwa unatamani awe mwezi wako. Hii itasaidia kuepuka maumivu ya kusiisha mahusiano yenu.
3. Pata uchunguzi wa kitabibu ili kuona kama kuna/hakuna dalili za vinasaba vya ulemavu.

Kwa ujumla, ulemavu si dhambi. Unaweza kumpata mtu yeyote. Kwa hakika hakuna mtu anayeweza kuepuka ulemavu kwa asilimia 100. Mtu akijaliwa kuufikia uzee wema lazima viungo kama macho na masikio vikose ufanisi wake. Ndio maana wazee wengi huanza kupata shida ya kuona na kusikia.

Ulemavu unahusika sana na mazingira matatu ya binadamu; yaani, kabla ya kuzaliwa, wakati wa kuzaliwa na baada ya kuzaliwa. Na kila mazingira ya vihatarishi husika kwa aina moja au zaidi ya ulemavu.

Nihitimishe kwa kusema kuwa hizi ni baadhi ya tahadhari miongoni mwa nyingi. Nyingine unazifahamu mwenyewe kutokana na mazingira yako. Pia tunayazungumza haya kutokana na matokeo ya athari za ulemavu kwenye maisha yetu sisi binadamu. Kikubwa zaidi ni hizi tamaduni zetu zinazotugawa kwa kuangalia maumbile ya binadamu.

Tufikiri Kijumuishi.....Tutende Kijumuishi.....Tujenge Taifa Jumuishi