Friday, May 16, 2025

Vifaa Saidizi Kwa Watoto Wasioona

 



Umuhimu wa Vifaa Saidizi kwa Wanafunzi Vipofu katika Muktadha wa Elimu Jumuishi

Katika muktadha wa elimu jumuishi, upatikanaji wa vifaa saidizi kwa wanafunzi wenye ulemavu wa kuona ni suala lenye uzito mkubwa. Uwepo wa vifaa hivi si suala la hiari bali ni haki ya msingi ya kielimu kwa kila mtoto. Wanafunzi vipofu wanapopewa vifaa vinavyowawezesha kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kujifunza, huweza kuimarika kitaaluma, kijamii na kisaikolojia kama ilivyo kwa wenzao wasio na ulemavu. Insha hii inajadili aina za vifaa saidizi vinavyohitajika kwa wanafunzi vipofu, umuhimu wake, pamoja na wajibu wa wadau mbalimbali katika kuhakikisha vifaa hivyo vinapatikana.

Kwanza, kuna aina mbalimbali za vifaa saidizi vinavyotumika kuwasaidia wanafunzi vipofu katika kujifunza. Miongoni mwa vifaa hivi ni vifaa vya kusomea na kuandikia kwa maandishi ya Braille kama vile mashine ya Perkins Brailler, karatasi maalum za Braille, na vitabu vya Braille. Vifaa hivi huwezesha wanafunzi kuandika na kusoma kwa kutumia mfumo wa hisia za vidole. Vifaa vya teknolojia ya kisasa pia ni muhimu, kama vile kompyuta zenye programu za kusoma maandishi kwa sauti (mfano JAWS, NVDA, VoiceOver), vifaa vya kurekodi na kusikiliza masomo, pamoja na simu janja au tablet zenye programu maalum za elimu kwa walemavu wa kuona. Aidha, vifaa vya mawasiliano na urambazaji kama saa za Braille, fimbo nyeupe za kujielekeza, na ramani za kielelezo kwa hisia husaidia wanafunzi kujiendesha kwa uhuru zaidi katika mazingira ya shule.

Umuhimu wa vifaa hivi hauwezi kupuuzwa. Kwanza, huwawezesha wanafunzi vipofu kujifunza kwa uhuru bila kutegemea sana msaada wa watu wengine. Pili, vifaa hivi huchangia katika kukuza usawa na ujumuishaji katika elimu, kwa kuwa vinawawezesha wanafunzi hawa kushiriki ipasavyo darasani kama wenzao. Tatu, vinachangia katika kuwajengea wanafunzi kujiamini, hasa wanapoweza kufanya kazi zao kwa kujitegemea. Vilevile, vinasaidia kuongeza ufaulu wa kitaaluma, kwani wanafunzi wanakuwa na fursa bora ya kuelewa masomo yao. Mwisho, vifaa hivi huimarisha mawasiliano, kwa kuwa vinawawezesha wanafunzi kuwasilisha mawazo yao kwa maandishi au kwa njia ya sauti.

Hata hivyo, upatikanaji wa vifaa hivi hauwezi kufanikishwa bila ushirikiano wa wadau mbalimbali wa elimu. Serikali ina wajibu mkubwa wa kuweka bajeti maalum kwa ajili ya vifaa saidizi, kushirikiana na mashirika ya kimataifa kutafuta msaada, pamoja na kutunga sera za elimu jumuishi zinazozingatia mahitaji ya wanafunzi wenye ulemavu. Wazazi na familia nao wanapaswa kuwahamasisha watoto wao kutumia vifaa hivyo, kushirikiana na walimu kutoa taarifa muhimu kuhusu watoto wao, na kuwezesha mazingira ya nyumbani kuwa rafiki kwa ujifunzaji. Walimu, kama watekelezaji wa sera ya elimu darasani, wana jukumu la kujifunza kutumia vifaa hivyo, kuandaa maudhui ya kufundishia yanayomfaa mwanafunzi kipofu, na kuhakikisha ushirikishwaji wa wanafunzi hawa katika kila shughuli ya kielimu.

Zaidi ya hapo, asasi zisizo za kiserikali (NGOs) na mashirika ya misaada yanapaswa kushiriki kikamilifu kwa kutoa vifaa, kutoa mafunzo kwa walimu na wazazi, na kuelekeza jamii juu ya umuhimu wa elimu jumuishi. Mwisho, jamii kwa ujumla wake ina wajibu wa kuchangia kwa hali na mali kusaidia shule au miradi inayowalenga wanafunzi vipofu, pamoja na kuunda mazingira ya kijamii yanayowaunga mkono.

Kwa kumalizia, vifaa saidizi kwa wanafunzi vipofu si anasa bali ni mahitaji ya msingi ya kujifunza. Elimu jumuishi haiwezi kufikiwa kikamilifu bila kuhakikisha kwamba kila mwanafunzi, bila kujali ulemavu wake, anapata fursa sawa ya kujifunza. Ni wajibu wa kila mdau wa elimu kushirikiana ili kuhakikisha vifaa hivi vinapatikana kwa wakati na kwa ubora unaohitajika. Kupitia ushirikiano huu, jamii yetu itaweza kujenga misingi ya usawa, heshima, na maendeleo kwa wote.

Wajibu wa Asasi za Kiraia kuwasaidia watu wenye ulemavu


Taasisi ya #Brighten Tanzania yatoa Msaada kwa Bima za Afya na Magodoro kwa watoto wenye Ulemavu Mvomero 

Link: https://web.facebook.com/share/p/16WWq5J6vE/









Saturday, June 8, 2019

Habari za Ulemavu

Stadi za Kujiajiri ni Muhimu kwa kila mtu


...kila mtu mwenye ulemavu ana uzoefu fulani wa kupitia njia nyembamba ya kufanikiwa...

1. Ulemavu unaweza kumpata mtu yeyote, wakati wowote na mahali popote.
2. Usiwe kikwazo kwa mtu mwenye ulemavu. Kama humsaidii kwa lolote basi usimzuilie maendeleo yake..
3. Asili ya ulemavu ni sehemu ya haiba tu.
4. Binadamu aliyezaliwa na binanadamu ni binadamu tu; na ana haki ya asili kwa kuwa amezaliwa binadamu...
5. Usipime uwezo wa kufanya kazi kwa mtu mwenye ulemavu kwa kuhisi, kudhani, au kwa mihemko ya aina yeyote. Jipe muda wa kutosha kufanya uchunguzi...
6. (a) Wewe binafsi unamchukuliaje mtu mwenye ulemavu, mzazi mwenye mtoto mwenye ulemavu?
(b) Unadhani ulemavu ni wa watu fulani fulani tu?
(c) Unajisikiaje au unapata hisia gani ukikutana na mtu mwenye ulemavu?

Tushirikishane katika maisha haya yenye mrengo wa ushirikishaji...
Asanteni kwa kusoma ujumbe...

Image result for ulemavu wa macho
Mwanamke Msusi ambaye ni kipofu.

Tuesday, April 17, 2018

TUJIFUNZE KUZUIA ULEMAVU USITOKEE

Image result for mama mjamzito 



Ulemavu unapatikana kupitia njia mbili tu
1. Kurithi
2. Mazingira

1. Ulemavu wa kurithi unaweza kuwa changamoto kuuzuia, japo mtu akifuata kanuni za kitabibu anaweza kuepuka. Mfano mmojawapo wa kuepuka hili ni kuepuka kuwa na ndoa na mtu wako wa karibu kiukoo (mtoto wa shangazi, mjomba, mama mdogo, mama mkubwa, baba mdogo, nk.)

Kabla ya kuoa / kuolewa onana na madaktari kwa ushauri wa mambo ya kiafya.

2. Ulemavu unaotokana na mazingira

Ulemavu utokanao na mazingira unajumuisha matukio yote yanayoweza kusababisha mtoto akazaliwa na ulemavu tangu kutungwa kwa mimba hadi kuzaliwa kwake huyo mtoto.

Baada ya kuzaliwa pia mtu anaweza akapata ulemavu kwenye mazingira yake ya kila siku.

Kama mama mjamzito, punguza uwezekano wa ulemavu kwa njia zifuatazo:
i. Pata lishe bora sawa na maelekezo ya madaktari.
ii. Hudhuria kliniki zote za kitabibu.
iii. Fuata maelekezo yote ya madaktari juu ya ujauzito.
iv. Pata kinga zote za kitabibu.

Baba mzazi jukumu lako ni:
i. Usimpige mkeo akiwa mjamzito.
ii. Usimfokee mara kwa mara mkeo mjamzito.
iii. Hakikisha mkeo mjamzito anapata lishe inayostahili.
iv. Mfanyie urafiki mkeo mjamzito ili kujenga maono (emotions) mema kwa mtoto.
v. Usimfanyie vitisho vyenye kuleta hofu na woga.
vi. Mpende mkeo mjamzito.


Baada ya kuzaliwa mtoto alindwe na hatari zozote hadi atakapokuwa na uelewa wa jema na baya kwa akili yake mwenyewe.

Uwe  na wakati mwema!

Monday, April 16, 2018

KUONGEZA THAMANI YA MTU MWENYE ULEMAVU

Image result for wajasilia mali wenye ulemavu 




Siku zote ulemavu huambatanishwa na matukio yote mabaya. Mtu mwenye ulemavu hufikiriwa kuwa ni masikini, asiyejiweza, naam, mtu tegemezi katika kila nyanja ya maisha ya mwanadamu. Hii dhana ni potofu, yafaa kukanushwa kwa nguvu zote, iwe kwa kuandika makala kwenye magazeti, kwenye vitabu, mihadhara, vipindi vya radio, tv na hata kwenye mitandao ya kijamii.

Hii dhana potofu kwenye jamii juu ya watu wenye ulemavu imeleta madhara katika mfumo wa maisha ya mtu mwenye ulemavu kwenye jamii. Moja ya madhara makubwa ni kuliona kundi hili ni jamii ya pili isiyo na thamani kwa kila kitu.

Njia za kuwaongezea thamani watu wenye ulemavu
1. Kuwafundisha watu wenye ulemavu kutumia vipaji vyao kujikwamua kiuchumi.
2. Kuwafundisha kujiamini
3. Kuwaeleza haki zao za msingi
4. Kuwachangamanisha na jamii nzima inayowazunguka.
5. Kuweka msisitizo wa elimu kwa watoto wote wenye ulemavu.


Tufikiri kijumuishi ~~ Tutende Kujumuishi ~~ Tujenge Taifa Jumuishi

Wednesday, September 20, 2017

HATUA NGUMU ANAZOPITIA MTU APATAYE ULEMAVU AKIWA AMEZALIWA




Kwa kawaida mtu akipata ulemavu akiwa amezaliwa huwa kuna kipindi cha mpito kiitwacho kipindi cha giza. Tuchukulie mfano wa mtu anayepata ukiziwi baada ya kuzaliwa.
Uzoefu unaonesha kuwa lazima hatua kadhaa zipitiwe.
1. Hatua ya kuukataa ulemavu (hawakubaliani na hali ya ulemavu).
2. Kwenda hospitali kwa uchunguzi
3. Wanaenda kwa mganga wa kienyeji kama matokeo ya hospitali si mazuri.
4. Kwenda kanisani au msikitini kulingana na imani yake kwa imani kuwa atapata uponyaji.

Wakifika mahali hapa kuna jambo moja kati ya mawili huweza kutokea:
(i) Kuishi maisha ya huzuni kama hawatakubaliana na hali ya ulemavu. Familia na jamii nzima huona ni msalaba mzito. Hawana la kujifunza zaidi ya kujihisi wamekataliwa na jamii nzima.
(ii) Kuishi maisha ya uhuru baada ya kupitia uzoefu mwingi wa athari za ulemavu. Wataishi kwa akili nyingi, kuwa karibu na jamii, kujitengenezea utamaduni mpya ambao ni jumuishi ndani ya familia.
Tujifunze mambo yanayohusu ulemavu kwa faida zetu wenyewe.

Thursday, September 14, 2017

JINSI YA KUMCHUNGUZA MWANAO KUONA KAMA ANA ULEMAVU AU LA

Image result for club foot 


Ulemavu unaweza kuwa wa kuonekana wazi wazi au ni ule usio wa wazi sana.

Mtoto akiwa angali mdogo unaweza kumchunguza mwenyewe.

1. Mchunguze maumbile yake ya nje (physical appearance), ukigundua kuna kasoro nenda kwa madaktari uone watakuelekeza kitu gani. Kwa mfano ukagundua ana Mguu Kifundo (Club Foot), huo ulemavu unaweza kurekebishwa ili kupunguza makali ya ulemavu.

2. Mpigie makelele ukiwa mahali ambapo hahisi uwepo wapo, akistuka ujue masikio yake yako vizuri, la sivyo, endelea na uchunguzi kwa madaktari.

3. Mtoto akifikisha umri wa kuanza kuhisi mwanga (light perception) pitisha viganja vyako karibu na macho yake, akistuka yuko vema, tofauti na hapo mpeleke kwa daktari.


Wazazi tuzingatie haya ili kupunguza athari za ulemavu kwa maisha ya watoto wetu.