Sunday, April 10, 2016

JE, WAJUA ATHARI ZA ULEMAVU KWA MAISHA YA MTU?




Kwa asilimia kubwa, ulemavu wenyewe sio tatizo, bali mtazamo wa jamii juu ya ulemavu huo ndio tatizo kubwa zaidi. Ukiacha ulemavu unaohusisha ubongo, ulemavu mwingine wote una faida ya kumwongezea akili nyingi mhusika mwenye ulemavu. Anakuwa na maisha ya utafiti wa kila siku juu ya tabia za binadamu na utamaduni wao. Ulemavu unaleta hamasa ya ugunduzi wa asili wa binadamu na tabia zake.
Hata hivyo, maisha ya ulemavu yamejaa kuanguka na kusimama kwa nyakati tofauti kutokana na tamaduni kinzani juu ya ulemavu na watu wenye ulemavu. Nafsi rahisi (easy minds) za watu wenye ulemavu na washirika wao huanguka kwa anguko kubwa kwenye maisha ya kila siku. Hii inatokana na uzito na ugumu wa taratibu za mila na desturi kwenye jamii zetu. Pia kumbuka kuwa ukiona mtu shujaa mwenye ulemavu kwenye kila jambo ujue kapigana kwa nguvu zana ili kushinda mapito hayo. Mtu mwenye ulemavu hukutana na maneno makali yenye kukatisha tama, vitendo vya ukinzani, mitazamo kinzani kama tufani ya bahari, kila hatua ya makuzi na maisha yake ni ukinzani tupu. Ndio maana kuna makabila fulani ya kitanzania wakiona dalili ya ulemavu kwa mtoto mchanga wanamuua siku ile ile ya kwanza kwa kisingizio kuwa si “riziki”.
1. Athari ya kiuchumi
Familia nyingi zenye watoto wenye ulemavu, hasa wa akili zinakumbwa na ugumu kiuchumi kwa kuwa muda mwingi wanatakiwa wawe na watoto wao wenye ulemavu. Hali hii inapelekea wazazi hao kuacha kazi zao za kiuchumi. Zipo shuhuda nyingi kwa watu ambao nimepata kuongea nao wenye watoto wenye ulemavu.
2. Athari za kijamii
Jamii zetu zina mtazamo hasi juu ya ulemavu. Mtu mwenye ulemavu amekosa sifa kwenye jamii, anaonekana ni mtu tegemezi, hana haki, mnyonge, amelaaniwa na matokeo yake ni kutengwa na jamii yake. Nimeona watu wengi ambao kabla ya kuwa na ulemavu walikuwa maarufu kisiasa, kiuchumi na kijamii, lakini mara walipopata ulemavu “status” zao zilibadilika.
3. Athari za kimazingira
Watu wenye ulemavu wa aina mbalimbali wanatakiwa watengenezewe njia wezeshi kwa maisha yao, yaani “deviated programs and means for people with disabilities”. Tumepungukiwa vifaa jumuishi. Mazingira mengi ya watu wenye ulemavu ni changamoto.
4. Sera za nchi
Zipo sera za watu wenye ulemavu na zingine kama miongozo kwa maisha ya wananchi kwa ujumla. Sera za watu wenye ulemavu ni ngumu kutekelezeka, na zile jumla hazina dalili ya ukaribu na mtu mwenye ulemavu.
Ushuhuda: Kuna rafiki mmoja ambaye ni mwalimu kipofu. Aliomba kazi ya kufundisha kwenye shule ya binafsi, kwa vile ufaulu wake ulikuwa mzuri walimwita kwenye usaili. Alipofika wakamwona kipofu, wakamwambia kwa kimombo”we need a teacher but not you, sorry for that.” Wakaongeza kusema: “Hatukujua kama wewe ni kipofu”.
Kiukweli ipo mifano mingi ya aina hiyo!
5. Utu wa mtu mwenye ulemavu
Fanya jaribio la uchunguzi: Fuatilia mahali ambapo ghafla ametokea mtu mwenye ulemavu usikie maneno ya watu juu yake. Hata kama hawasemi chochote utaona “facial expressions” zao tu. Kiukweli utagundua ya kuwa kwa mitazamo ya jamii zetu mtu mwenye ulemavu anawekwa kwenye jamii ya upili. Kila mtu hufikiri ana mamlaka juu ya mtu mwenye ulemavu, mtu mwenye ulemavu hakui kwenye jamii, siku zote hufikiriwa ni tegemezi, ana akili za kitoto, na kila afanyacho huonekana si sahihi.
Ugumu kwa wapatao ulemavu ukubwani ni ile hali ya kuzoea aina mpya ya maisha. Marafiki hupungua, imani ya watu kwake hupungua. Hii hali huwafanya watu hawa wenye ulemavu kuishi maisha ya simanzi siku zote.
Ushuhuda
Mwanafunzi wangu mmoja wa zamani alipata ajali na kukatwa mguu (unyayo wote), amekuwa na mazingira magumu sana. Amekuwa ni mtu wa kutoa machozi tu akifikiria ugumu anaoupata.


Usione shida kwa msisitizo ambao huwa nautoa kila siku juu ya mambo ya watu wenye ulemavu. Ukichunguza kwa makini haya madhara ya mtu kuwa na ulemavu unakuta mtu asiye na ulemavu anaogopa neno “ulemavu” kuliko ulemavu wenyewe. Akisikia habari za ulemavu na watu wenye ulemavu anahisi masikio yanapata kuumia. Kwa hakika, ulemavu unamgusa kila mtu kwa namna yake.
Je, ulishawahi kujiuliza mapito ya watu albino nchini? Mapito ya watu albino na watu wenye ulemavu mbalimbali ndiyo sababu kubwa inayonifanya niendelee kuzungumzia masuala ya ulemavu kwa kadri Mungu anavyoniwezesha kuwa na uhai kwa manufaa yetu sote. Tujifunze juu ya ulemavu, tujifunze tunavyoweza kuishi na ulemavu na/au watu wenye ulemavu.

Tufikiri Kijumuishi…..Tutende Kijumuishi……Tujenge Taifa Jumuishi…

Muondolee mwanao athari za ulemavu

Maamuzi unayofanya leo juu ya mwanao ndiyo hatima ya maisha yake ya baadae. Maisha yake ya baadae yatakuwa ni matokeo ya maamuzi utakayomfanyia leo juu ya maisha yake. Maisha yetu ni matokeo ya maamuzi yaliyofanywa juu yetu na watu wengine.

Kabla ya kuzaliwa

Mama mjamzito afuate na kuzingatia maelekezo yote ya kitabibu juu ya ujauzito wake. Kula vyakula stahiki na fanya mazoezi sahihi kwa makuzi bora ya mtoto tumboni. Upo uwezekano wa mtoto kuzaliwa akiwa na ubovu wa mifupa, kuharibika akili, kulemaa viungo nk.
Club foot (Kifundo mguu)

Wakati wa kuzaliwa
Fuata maelekezo ya madaktari ili mtoto wako azaliwe kwa wakati husika. Usisahau kumwomba Mungu ili awe nawe wakati huu. Mtoto akichelewa kuzaliwa kwa wakati na kwa kutumia vifaa saidizi kuna madhara ya kuharibiwa ubongo wake.

Wakati amezaliwa
Hakikisha unamlinda mwanao na vihatarishi vyote juu ya ulemavu unaoweza kumpata mwanao. Mfano: Epuka kumpa mwanao vifaa vyenye ncha kali kama sindano ambavyo vinaweza kutoboa macho na masikio, Epuka uwezekano wa kumwangusha mwanao (anaweza kulemaa akili na viungo), epuka kukaa na mwanao maeneo yenye kelele (ili kuepusha ukiziwi na kukosa utulivu-Hyperactivity). Epuka kumweka mtoto kwenye mchanga kama ule wa kupigia sakafu za nyumba. Ni hatari kwa macho ya mtoto. Upo ushuhuda mwingi juu ya watu waliopata upofu kupitia mchanga.
Pia mchunguze mwanao viungo vyake baada ya kuzaliwa. Kuna ulemavu uitwao "Club foot" au "Kifundo mguu" ambapo mtoto anakuwa na unyayo uliojikunja, matege yasiyo kawaida. Ukigundua mapema mpeleke mwanao hospitali kwa tiba zaidi.

Haya niliyoyataja na yale ambayo sikuyataja na mengine mengi unayoyafahamu yazingatie sana kwa ustawi wa maisha ya mwanao.

Msisitizo: Ulemavu una athari kubwa kwa mtu mwenyewe mwenye ulemavu, familia yake na hata ukoo wake. Athari hizi zinahusisha nyanja za kiuchumi, kisiasa, kijamii na kiutamaduni kwa ujumla wake.

Najiandaa kukuletea mada ya athari za ulemavu kwenye maisha!

Fikiri Kijumuishi.....Tenda Kijumuishi..... Jenga Taifa Jumuishi......

Unauelewaje Ulemavu?



Kwanza kabla ya yote niseme tu kuwa ukiona mtu anaelewa haraka juu ya mambo ya watu wenye ulemavu ujue kuwa kwa namna moja au nyingine aliwahi kupata aidha kwa ndugu wa karibu mwenye ulemavu na/au ana rafiki mwenye ulemavu.
Watu wengi ambao nimeongea nao inonyesha kuwa walishaguswa na huu ulemavu, iwe kwa watoto wake, wazazi wake, wenzi wao, na watu wao wengine ambao ni wa karibu sana. 

Nimegundua kuwa masuala ya ulemavu hayazungumzwi sana kwenye jamii kutokana na tamaduni zetu.
Watu wamefanya ulemavu kuwa ni siri kubwa. Watu wengi wenye ndugu zao wenye ulemavu wanawafungia ndani ndugu hao wenye ulemavu, wamewakosesha fursa ya elimu na haki ya kuchangamana na jamii. Hii ni kwa sababu elimu juu ya watu wenye ulemavu na ulemavu wenyewe haitiliwi mkazo. 

Watu wengi wakishindwa kutafsiri masuala ya ulemavu kitaalam hujikita katika imani za dini, na kishirikina. Wengi kwa imani huamini kuwa mtu kupata ulemavu ni laana ya ukoo. Wababa wengi wamewakimbia familia zao (wake wao wazaao watoto wenye ulemavu) zenye watoto wenye ulemavu.

Kwa hakika ulemavu umetafsiriwa na binadamu kwa ajili ya binadamu. Kila binadamu ni mhanga wa ulemavu. Tuvumiliane, tuheshimiane, tusaidiane inapobidi, tuuangalie uthamani wa binadamu na ubinadamu wake. Ulemavu ni sehemu tu ya haiba ya mwanadamu.

Je, una mtoto mlemavu?, rafiki mlemavu?, mzazi mlemavu?, mwenzi mlemavu? au wewe mwenyewe una ulemavu?

Usijali maneno na mitazamo ya watu wengine juu ya ulemavu huo. Ishi kwa kadri ulivyojizoeza!

Fikiri Kijumuishi...Tenda Kijumuishi....Jenga Taifa jumuishi!

Sunday, March 13, 2016

Tupunguze viashiria vya ulemavu

Katika dunia ya leo, asilimia kumi ya kila idadi ya watu kadhaa ni watu wenye ulemavu.
Ulemavu upo wa makundi mawili,; wa kuzaliwa nao (congenital) na ule aupatao mtu akiwa amezaliwa (acquired). Pia ulemavu unaweza kuwa wa kurithi kutokana na vinasaba vya mtiririko wa kizazi husika.

(A) Namna ya Kupunguza ulemavu

Ulemavu wa kuzaliwa (ambao si wa kurithi)
1. Mama mjamzito fuata kanuni za kitabibu kwa kupata virutubisho sahihi kwa makuzi ya ujauzito wako
2. Baba epuka kuleta ghasia kwa mama mjamzito kama vile kumpiga mateke ya tumbo, kuwa mkali kwa mke wakati wa ujauzito wake.
3. Baba na mama mshirikiane ili kuhakikisha mimba inakua vizuri hadi hapo mtoto atakapozaliwa
4. Daktari awe wazi kuwataarifu wazazi watarjiwa wa mtoto pale anapobaini kuna dalili za ulemavu kwa mtoto ili kuona kama uwezekano wa kupunguza athari za ulemavu huo. Mfano, mtoto anayezaliwa na kifundo cha mguu (Club foot) anaweza kurekebishwa miguu yake angali mtoto mchanga.
5. Baba na mama muishi maisha ya furaha, hasa baba jitahidi kumjengea mama mjamzito furaha kubwa.

(B) Ulemavu baada ya kuzaliwa
Ulemavu wa aina hii ni matokeo ya ajali mbalimbali kwenye mazingira yetu
1. Epuka kugongeshagongesha kichwa cha mtoto mchanga ili kuepuka kuharibu ubongo wa mtoto (mtindio wa ubongo)
2. Epuka kukimbilia kwa waganga wa kienyeji kwa tiba isiyo ya lazima kwa watoto. Kituo cha kwanza kwa matibabu yoyote ya mtoto iwe kwa madaktari waliosomea udaktari. Huko kwingine iwe ni ziada tu (hii itasaidia kitaalam kujua maendeleo ya afya ya mwanao.
3. Epuka kumpa mtoto wako vifaa vyenye ncha kali kama vile sindano, mouth sticks, kalamu za wino, visu nk. Vifaa hivi ni hatari kwa macho na masikio ya mtoto (upofu na ukiziwi au vyote kwa pamoja).
4. Epuka kumweka mwanao kwenye mchanga. Mara nyingi ni hatari kwa macho ya mtoto.
5. Epuka kumtishia mtoto mdogo kama vile tusemavyo kwa vitisho. Hii huweza kumsababishia mtoto kuwa na vurugu za maono, hasa hasira na woga uliopitiliza kiasi cha asili ya binadamu.
6. Epuka kumpiga makofi mwanao; unaweza ukamharibu masikio na mishipa ya macho na kumsababishia upofu na ukiziwi.
7. Epuka kuishi maeneo yenye kelele nyingi kama vile viwandani, migodini, vituo vya mazoezi ya kulenga shabaha kwa wanajeshi, karibu na viwanja vya ndege. Hii husababisha ukiziwi kwa mtoto.

(C) Ulemavu wa kurithi
Hapa sasa niongee na vijana ambao hawako kwenye ndoa.
Mara nyingi ulemavu wa kurithi ni matokeo ya kuwepo kwa vinasaba vya ulemavu husika kwa wana ndoa.
Ili kuepuka na/au kupunguza huu ulemavu ni jukumu lako kijana ambaye hujaoa au kuolewa kufanya uchunguzi wa kina juu ya mwezi wako mtarajiwa.
1. Uliza kama kwenye ukoo wao kuna ulemavu wa kurithi, na kama upo, je, unaweza ukaathiri kizazi chenu? Upo ulemavu wa kurithi ambao akiwa nao mmoja wa wana ndoa hauwezi kuathiri kizazi chenu.
2. Anza maandalizi ya uchunguzi wa huyo unayependa awe mwezi wako kabla ya kumdokezea kuwa unatamani awe mwezi wako. Hii itasaidia kuepuka maumivu ya kusiisha mahusiano yenu.
3. Pata uchunguzi wa kitabibu ili kuona kama kuna/hakuna dalili za vinasaba vya ulemavu.

Kwa ujumla, ulemavu si dhambi. Unaweza kumpata mtu yeyote. Kwa hakika hakuna mtu anayeweza kuepuka ulemavu kwa asilimia 100. Mtu akijaliwa kuufikia uzee wema lazima viungo kama macho na masikio vikose ufanisi wake. Ndio maana wazee wengi huanza kupata shida ya kuona na kusikia.

Ulemavu unahusika sana na mazingira matatu ya binadamu; yaani, kabla ya kuzaliwa, wakati wa kuzaliwa na baada ya kuzaliwa. Na kila mazingira ya vihatarishi husika kwa aina moja au zaidi ya ulemavu.

Nihitimishe kwa kusema kuwa hizi ni baadhi ya tahadhari miongoni mwa nyingi. Nyingine unazifahamu mwenyewe kutokana na mazingira yako. Pia tunayazungumza haya kutokana na matokeo ya athari za ulemavu kwenye maisha yetu sisi binadamu. Kikubwa zaidi ni hizi tamaduni zetu zinazotugawa kwa kuangalia maumbile ya binadamu.

Tufikiri Kijumuishi.....Tutende Kijumuishi.....Tujenge Taifa Jumuishi

Monday, March 7, 2016

Improved Access for People with Disabilities



Why do we need to ensure access for people with disabilities?



 In many countries, it is the law.
Many countries have either passed specific laws concerning the rights of people with disabilities, or have enshrined those rights in their constitutions.

It is a matter of fairness and respect.
People with disabilities have the same rights as others, including the right to fully participate in community life. Everybody has a right to live as normal a life as possible.

Failing to do so wastes talent and energy.
Many people with disabilities in all walks of life are competent at important jobs, and some do remarkable work. Denying people access to employment, education, or services wastes human resources and makes society poorer.

It makes good business and economic sense.
 For commercial operations of any kind, accessibility means that people with disabilities can become customers, increasing sales volume and profits.  Furthermore, if a firm is a good place for customers with disabilities to do business, the word will get around.

Many people with disabilities already have a difficult life.
It’s simple human decency not to make it any harder than necessary.
People with disabilities add to the diversity of the community, and that diversity makes everyone’s life richer. If they can mix normally with the rest of the community, they will have more friends and acquaintances, and more people will have the opportunity to know them.

Access for people with disabilities improves access for everyone.
 Making public spaces and facilities physically accessible for people with disabilities also makes them more accessible for people who may not have disabilities, including families with baby strollers, skateboarders, and bicycle riders. Making ramps a built-in feature of the environment is good for everyone.

Think Inclusively... Act Inclusively..... Build an Inclusive Nation

Thursday, February 18, 2016

NAFASI YA WATU WENYE ULEMAVU KWENYE JAMII

Ninapenda sana kuzungumza habari za ulemavu na watu wenye ulemavu. Hii si kwa sababu zinapendeza na kufurahisha mioyo ya wengi, bali ni habari ambazo zinahitajika sana kwa wakati uliopo kwa ukombozi wa fikra, nafsi na mitazamo ya watu kwenye jamii zetu. Huwezi kupata vionjo kamili vya moyo na hisia juu ya athari za ulemavu hadi uguswe na ulemavu; kwa maana ya kwamba wewe mwenyewe uwe na ulemavu na/au uwe na mwanafamilia mwenye ulemavu.

Nimesoma vitabu vingi, majarida mengi na magazeti pia. Nimeona jinsi jamii zetu zinavyojitahidi kuchambua habari ya ulemavu na watu wenye ulemavu. Jambo moja kuu katika maandiko yote hayo waandishi huishia kuwajengea watu hisia za huruma bila kutaja wazi wazi na kwa ujasiri uthabiti wa watu wenye ulemavu kwenye jamii zao. 

Ulemavu unaweza kumpata mtu yeyote kwenye maisha wakati wowote na mahali popote.

Biblia imemtaja mjukuu wa mfalme Sauli, yaani mtoto wa Yonathani kuwa alikuwa mlemavu.

2Samweli 4:4
"Naye Yonathani, mwana wa Sauli alikuwa na mwana aliyekuwa na kilema cha miguu.....Na jina lake aliitwa Mefiboshethi."

Makazi ya watu wenye ulemavu

1. Makazi katika ardhi
Mazingira mengi ya watu wenye ulemavu wanaishi kwenye mazingira mabaya na magumu, mazingira yasiyosadifu maisha ya maendeleo.
Mfano, mjukuu wa mfalme Sauli aliwekwa katika eneo lililoitwa Lo-Debari.
Lo-Debari- ni eneo lisilo na malisho, eneo lenye ugumu wa kuishi. Kwa mantiki hii watu wengi wenye ulemavu wanaishi Lo-Debari zao katika nchi zao.

2. Fahamu zetu zinawaweka mahali gani watu wenye ulemavu?
Hata wewe ni shahidi, watu wenye ulemavu wamefikiriwa kuwa ni watu wasio na faida kwenye jamii zetu. Adolf Hitler wa Ujerumani kwa kupitia dhana hii aliwaita watu wenye ulemavu kuwa ni USELESS EATERS (walaji wa rasilimali za jamii wasio na faida (see Eugenic Movement: The War Against the Weak).

3. Mamlaka za watu wenye ulemavu ziko wapi?
Kwa utamaduni wa binadamu Tanzania na dunia nzima kwa ujumla zinaonyesha kuwa watu wenye ulemavu wanatawaliwa na kila mtu. Hii ndiyo dhana ya watu wengi. Utamkuta mtu mwenye ulemavu msomi, ana pesa, ana ufahamu wa mambo mengi ambayo yangekuwa msaada kwa wengi. Kinyume chake utakuta kila mtu asiye mlemavu anahisi yeye ndiye mtawala wa mtu mwenye ulemavu. Ushahidi ni pale utakapoona mtu mwenye ulemavu akisemwa na kusimangwa na kila mtu, na hata pengine huwa na kuzushiwa na kusingiziwa tu.
4. Tujifunze kwa mfalme Daudi

"1  Kisha Daudi akasema, Je! Amesalia mtu mmoja katika nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema kwa ajili ya Yonathani?
2  Palikuwa na mtumishi mmoja wa nyumba ya Sauli, jina lake Siba, basi wakamwita aende kwa Daudi; na mfalme akamwuliza, Wewe ndiwe Siba? Naye akasema Mimi, mtumwa wako ndiye.
3  Mfalme akasema, Je! Hakuna hata sasa mtu ye yote wa nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema ya Mungu? Siba akamwambia mfalme, Yonathani anaye mwana hata sasa, aliye na kilema cha mguu.
4  Mfalme akamwambia, Yuko wapi? Siba akamwambia mfalme, Tazama, yumo katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari.
5  Basi mfalme Daudi akatuma watu, akamwondoa katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari.
6  Basi Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli akaenda kwa Daudi, akaanguka kifudifudi, akasujudu. Daudi akasema, Mefiboshethi! Naye akaitika, Mimi hapa, mtumwa wako!
7  Daudi akamwambia, Usiogope, maana bila shaka nitakutendea mema; kwa ajili ya Yonathani, baba yako, nami nitakurudishia mashamba yote ya Sauli, baba yako; nawe utakula chakula mezani pangu daima.
8  Akasujudu, akasema, Mimi mtumwa wako ni nini, hata ukamwangalia mbwa mfu kama mimi?" 

MANENO MAGUMU HAYA
2Samweli 9:8 
 "Akasujudu, akasema, Mimi mtumwa wako ni nini, hata ukamwangalia mbwa mfu kama mimi?" 

Siku zote ukitaka kujua mtu alikuwa na mazingira magumu kabla ya kusaidiwa fuatilia "SHUKRANI ZAKE". Huwa ni za kipekee sana. Soma 2Sameli 9:8 ujionee.

NIONAVYO
Watu wenye ulemavu wamepitia, naam, wanaendelea kupitia kwenye mazingira magumu. Shida za watu wenye ulemavu zinafanana kote duniani zikiwa kwenye vipengele vya Miundo mbinu, Mtazamo wa jamii na mawasiliano. Tujitahidi kujenga jamii jumuishi ili tuishi kwenye taifa ambalo halimtengi mtu kwa namna yoyote ile. Nikumbushe pia kuwa leo mtu ambaye ndiye kikwazo kwa mtu mwenye ulemavu ndiye pia anaweza akawa kwenye orodha ya watakaopata ulemavu muda mfupi ujao. Jumuisha ili ujumuishwe.

FIKIRI KIJUMUISHI~~~ TENDA KIJUMUISHI ~~~ JENGA TAIFA JUMUISHI

Saturday, February 6, 2016

WALIMU WA ELIMU MAALUM NA WANAFUNZI WA ELIMU MAALUM WAKUTANE SHULENI





Mwanafunzi mwenye mahitaji maalum anamhitaji mwalimu mwenye taaluma ya elimu maalum; pia mwalimu wa elimu maalum anamhitaji mwanafunzi mwenye mahitaji maalum. Ni mtegemeano wa aina yake.


Tanzania, kama nchi zingine duniani, ina wanafunzi wenye mahitaji maalum. Pia ni bahati iliyoje kuwa na vyuo vyenye kutoa elimu maalum kwa walimu ili kukidhi mahitaji maalum ya wanafunzi hao wenye mahitaji maalum.

Hata hivyo kuna kila dalili ya kushuka kwa huduma za elimu maalum nchini Tanzania. Walimu wengi wanaomaliza kozi za vyuo vya elimu maalum wamekuwa wakipangiwa shule za kawaida (normal schools) zenye watoto wasio na mahitaji maalum.

Kwa upande mwingine wanafunzi wenye mahitaji maalum nchini wameendelea kuwepo mitaani bila kwenda shule kwa kigezo kuwa hakuna walimu wa kuwafundisha hawa watoto.

Elimu jumuishi bila mipango inaumiza wachache.


HOJA

Walimu wenye fani ya elimu maalum wapelekwe kwenye shule maalum za watoto wenye mahitaji maalum; sambamba ni hilo, pia kuanzishwe shule maalum kwa watoto hao kwenye maeneo yasiyo na shule hizo. Zipo wilaya nyingi zisizo na shule maalum, mfano halisi ni wilaya ya Mvomero, haina shule za viziwi na wasioona.